Sitti Mtemvu apokelewa kifalme Morogoro!!!

MSHIRIKI wa Shindano la Miss Tanzania mwaka 2014, aliyeshinda taji hilo katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam na baadaye kuthibitika kuwa alighushi umri na hivyo kulitema na kusababisha kufungiwa kwa shindano hilo, Sitti Mtemvu, juzikati alipokewa kama mfalme alipofanya ziara fupi mjini Morogoro.

 
Mshiriki wa Shindano la Miss Tanzania mwaka 2014 Sitti Mtemvu.

Mrembo huyo ambaye hivi sasa anaongoza taasisi yake inayofahamika kama Sitti Tanzania 2015, alipofika mjini hapa, baadhi ya mashabiki wake walijipanga kutokea eneo la Nanenane na kuambatana naye hadi katika hospitali ya mkoa ambako alitoa msaada wa vyandarua katika wodi ya wazazi.

Baada ya kukabidhi misaada hiyo, mrembo huyo ambaye baba yake mzazi ni Mbunge wa Jimbo la Temeke, alikwenda hadi ofisi za Chama cha soka mkoani hapa na kutoa msaada wa mipira mitano na seti moja ya jezi kwa lengo la kusaidia kuimarisha michezo.

“Najisikia vizuri sana nimepokelewa kama mfalme, kundi la wananachi wa Morogoro walijipanga maeneo ya Nanenane ambapo walinipokea, binafsi sikutarajia kukutana na mapokezi kama haya, mimi ni Mluguru na nimekuja kwetu Morogoro kuwasaidia watu wenye uhitaji mbalimbali,” alisema binti huyo baada ya kumaliza shughuli zake.

Lakini katika hali ya kushangaza, alipoulizwa kuhusu anavyojisikia baada ya kulitema Taji la Miss Tanzania, Sitti alijibu kwa mkato; “Sijisikii vibaya na wala sitaki kuzungumza ishu ya Miss Tanzania,” alisema na kukatisha mahojiano hayo hapohapo kabla ya kuingia kwenye gari lake bila hata kumuaga mwandishi