Kabla ya Uchaguzi Mkuu Mangula Aamua Kuwasaka Wasaliti CCM..Adai Kila MTU awe Mlinzi wa Mwenzie Kwani CCM imejaa Wasaliti


MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Philip Mangula amemaliza ziara yake katika majimbo ya Mkoa wa Dar es Salaam, na kuagiza kila mwanachama awe mlinzi wa mwenzake, amchunguze ili kuepuka wasaliti.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mangula alisema kuna wanachama wamekuwa wakikisaliti chama hicho tangu mwaka 2010 na wengine bado wapo, ambao wamekuwa wakisababisha CCM kushindwa uchaguzi katika baadhi ya maeneo.

Kila mtu awe mlinzi na ukigundua kwamba kuna anayesaliti chama atoe taarifa na atakapobainika kweli ni msaliti atafukuzwa ndani ya chama... CCM ina viongozi wengi kila mtu ni kiongozi ila nyakati za kuongoza zinatofautiana,” alisema.

Mkakati wa Ushindi Akizungumzia mkakati wa ushindi, Mangula alitaka wanachama wake kuhakikisha kwamba mgombea atakayesimamishwa anakuwa mgombea wa chama, ili kusaidia chama hicho kupata ushindi katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Tunaandaa chama chetu ili kupata ushindi, hivyo mgombea atakayesimamishwa atakuwa wa chama, kwa sababu kinaposhindwa chama hatusemi fulani kashindwa, bali chama kimeshindwa vivyo hivyo na mgombea akishinda ni ushindi wa chama.

Wakati wa kura za maoni ni wakati ambao mwanachama anagombea ili kuwakilisha chama na pale ndipo anakuwa na kundi, lakini baada ya mgombea kuteuliwa ni chama kinachogombea hivyo makundi yanatakiwa kuvunjwa na kumuunga mkono mgombea aliyeteuliwa, ili kukipatia chama ushindi.

Tunatakiwa kumpa ushirikiano mgombea wetu tutakayemsimamisha na tunahitaji nguvu ya ziada na kuunda umoja, ili kufanya mgombea wetu ashinde… mtu anatakiwa kutangaza sera za chama na siyo sera zake,” alisema Mangula.

Amani Aidha aliwaasa wanasiasa wasitumie mtego wa kuingia kwenye uchaguzi kuvuruga amani ya nchi, kwa kuwa katika nchi zote zilizo na machafuko, mara nyingi huchangiwa na baadhi ya wanasiasa na baadhi ya viongozi wa dini.

Pia aliwataka wana CCM kujipanga kuimarisha ulinzi katika vituo vya kupigia kura na kuweka tahadhari bila kupigana, ili kuepusha vurugu zinazochangia kura nyingi kupotea kutokana na watu kuogopa kwenda vituoni kwa kuhofia usalama wao.

Awali kabla ya kuzungumza na waandishi wa habari, Mangula alikutana na wajumbe wa Halmashauri ya CCM Mkoa wa Dar es Salaam. Naye Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Didas Masaburi alisema wametekeleza ilani ya CCM kwa vitendo katika miundombinu ya barabara, elimu na maji.

Mbali na mafanikio katika miundombinu hayo, Masaburi pia alisema wapo katika mchakato kuhakikisha kila Manispaa inakuwa na dampo lake ili kudhibiti usafi wa mazingira.