Shilole Alewa Chakari Ashuswa Kwenye Boti

Shilole
Staa wa Bongo Movies na Bongo Fleva, Zuwena Mohamed ‘Shilole’, juzikati alijikuta akilewa chakali kiasi cha kushindwa kupanda boti iliyokuwa imeandaliwa maalum kwa ajili ya kwenda kusherehekea tukio la kukatwa keki katika kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa ya msanii mwenzake, Estelina Sanga ‘Linah’, iliyofanyika Slipway, Masaki jijini Dar.

Shilole alikuwa amealikwa kwenye sherehe hiyo iliyoanza kurindima jioni ya saa 10 ndani ya Ukumbi wa Paparazi, ambapo waalikwa walianza kupata mapochopocho zikiwemo pombe na baadaye kutakiwa kupanda boti ili kwenda kumalizia sherehe katikati ya maji kwa kukata keki.

Kutokana na kubugia kiburudisho kupita kiasi, Shilole alishindwa kupanda boti iliyokuwa imeegeshwa pembeni mwa bahari na hivyo kumpa kazi ya ziada mchumba wake Nuh Mziwanda aliyelazimika kumrudisha garini ili warejee nyumbani.

“Kusema kweli mimi hata sielewi nilishindwaje kupanda boti, network ilikata, nilishangaa tu kujikuta nipo kwenye bethidei ya Menina Mikocheni, nafikiri kilichotokea muulize baby wangu Nuh Mziwanda,” alisema Shilole baada ya kuulizwa kuhusu ‘kuzimika’ kwake.

Nuh Mziwanda alikiri kuwa mpenzi wake alipoteza fahamu, kiasi cha kumlazimisha yeye kumbeba na kumrudisha tena klabu ya Paparazi ambako alipatiwa maji baridi kwa wingi huku akipigwa na kiyoyozi cha nguvu kabla ya kwenda kwenye shughuli ya Menina.

GPL