MBIO za mwamuzi, Ezekiel Ngoji,
wa Shinyanga juzi Jumapili zilimwokoa asipate kipigo cha nguvu kutoka
kwa wachezaji wa Polisi Dodoma baada ya kutokea vurugu kwenye mchezo wa
Ligi Daraja la Kwanza dhidi ya Toto African katika Uwanja wa Kirumba
jijini hapa.
Vurugu hizo ambazo zilifanya Polisi waliokuwepo uwanjani hapo kufyatua mabomu ya machozi kadhaa kuthibiti hali hiyo.
Awali mchezo ulianza vizuri lakini hali ilibadilika kipindi
cha pili kwenye dakika ya 63 baada ya mwamuzi Ngoyi kutoa penalti kwa
Toto kwa kile kilichoelezwa kipa wa Polisi Madopi Mwingira alimchezea
rafu mmoja wa washambuliaji wa Toto.
Penalti hiyo ilipigwa na Hamim Abdul ambaye alifunga na
sekeseke lilianza baada ya mwamuzi huyo kumtoa kwenye benchi mmoja wa
makocha wa Polisi na ndipo vurugu hizo zilipoanza kwa mmoja wa wachezaji
wa Polisi kuanza kumshambulia mwamuzi Ngoyi.
Baada ya kuona hivyo mwamuzi huyo alitimua mbio kuelekea
jukwaa kuu kujiokoa na kipigo hicho hali iliyowafanya askari waliokuwepo
uwanjani hapo kufyatua mabomu ya machozi kuzuia vurugu hizo.
Dakika 20 baadaye, waamuzi hao walitoka jukwaa kuu wakiwa na
maofisa wa Polisi na viongozi wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza(MZFA)na
kwenda uwanjani kupiga kipenga cha kumaliza pambano.
Kocha wa Polisi Dodoma, Gabriel
Marwa alisema mwamuzi wa mezani ndiye aliyeharibu pambano kwa kuwatoa
bila sababu kwenye benchi viongozi wenzake jambo lililosababisha hali
hiyo.